Monday, 9 November 2015

Ufaransa yaeleza wasiwasi kuhusu hali Burundi

Ufaransa imependekeza hatua zichukuliwe kusitisha mauaji ambayo yamekuwa yakiendelea nchini Burundi.
Taifa hilo liliwasilisha mswada wa mapendekezo kwa Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa Jumatatu likieleza wasiwasi wake kutokana na machafuko yanayoendelea nchini humo.
Machafuko hayo ndiyo mabaya zaidi nchini humo katika kipindi cha miaka kumi.
Ghasia zilianza Aprili baada ya maandamano ya kupinga hatua ya Rais Pierre Nkurunziza kutangaza angewania urais kwa muhula wa tatu. Jumamosi, watu tisa waliuawa kwa kupigwa risasi katika baa moja mji mkuu wa Bujumbura.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon alishutumu mauaji hayo ya Jumatatu na kusema mmoja wa waliouawa alikuwa afisa wa UN.
Afisa mmoja wa polisi anadaiwa kujeruhiwa na takriban watu wawili kuuawa huku polisi wakindelea kusaka silaha katika nyumba za wakazi mitaa ambayo ni ngome ya wapinzani.
Rais wa Rwanda Paul Kagame amekosoa viongozi wa Burundi kutokana na wanavyoshughulikia mzozo nchini humo na kuna wasiwasi huenda kukatokea mauaji ya kimbari, mwandishi wa BBC Alastair Leithead anasema.
Naibu balozi wa Ufaransa katika UN Alexis Lamek aliambia AFP kwamba Ufaransa “imehofishwa sana na yanayoendelea Burundi kwa sasa.”
Ujumbe wa Ufaransa katika UN ulisema mashauriano kuhusu azimio lake yangeanza Jumatatu jioni.
Shirika la International Crisis Group lenye makao yake Brussels limeonya kuwa lugha inayotumiwa kwa sasa Burundi “inashabihiana sana” na iliyotumiwa Rwanda kabla ya mauaji ya halaiki ya 1994.
Machafuko yalianza Aprili Nkurunziza aliposema muhula wake wa kwanza wa urais haukufaa kuhesabiwa katika kutekeleza takwa la kikatiba la rais kuhudumu mihula miwili pekee kwa kuwa alichaguliwa na wabunge wakati huo.

No comments:

Post a Comment